Saturday 1 March 2014

Nyerere alitaka Serikali tatu

Maelezo hayo ya Mwalimu Nyerere yapo kwenye kitabu chake cha Uongozi Wetu Na Hatima ya Tanzania kilichoandikwa mwaka 1994 na kutolewa 1995.
“Wakati Mwalimu anaandika kitabu hiki mwaka 1994 taifa letu lilikuwa linakabiliwa na changamoto kadhaa za kihistoria ambazo ndizo zilimfanya kuingilia kati na kuandika kijitabu hiki ambacho kilikuwa kama nasaha, onyo, na usia kwa Watanzania,” inasema sehemu ya utangulizi wa kitabu hicho.
Katika sura ya nne ya kitabu hicho, pamoja na mambo mengine Mwalimu Nyerere alizungumzia suala la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo alieleza sababu zilizofanya muungano wa serikali mbili ukaanzishwa.
“Labda ni vizuri kukumbuka kwamba shabaha ya baadhi yetu ilikuwa ni kuziunganisha nchi za Afrika Mashariki ziwe nchi moja,” alisema katika kitabu chake hicho.
Alieleza kuwa, wakati Zanzibar na Tanganyika zinaungana, Kenya, Uganda na Tanganyika zilikuwa katika mazungumzo ya kutafuta uwezekano wa kuungana.
“Kama jambo hilo lingetokea, nina hakika kabisa kwamba mfumo wa nchi mpya ambayo ingezaliwa ungekuwa ni wa shirikisho; ama shirikisho la nchi tatu zenye serikali nne, au shirikisho la nchi nne zenye serikali tano.
“Kwa kweli hata kesho nchi za Afrika Mashariki zikiamua kuungana na Tanzania ikawa ni mshiriki, naamini kuwa ni rahisi zaidi kushirikisha Tanzania yenye serikali mbili ya Zanzibar na ya Tanganyika kuliko Tanzania yenye serikali mbili, ya Tanzania na Zanzibar,” alisema.

No comments:

Post a Comment