Tuesday 1 April 2014

Mtoto Satrine atolewa risasi kichwani.

 Madaktari katika hospitali kubwa zaidi ya umma nchini Kenya,Kenyatta, wamefanikiwa kutoa risasi iliyokuwa imekwama katika ubongo wa mtoto Satrine Osinya mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu.

Risasi hiyo iliyomuingia mtoto Satrine kichwani ndiyo iliyomuua mamake.Mamake Satrine alikuwa amempakata mtoto wake ili kumlinda kutokana na magaidi waliovamia kanisa walimokuwa wiki moja iliyopita katika mtaa wa Likoni mjini Mombasa.Lakini walimpiga risasi mama huyo na kumuua papo hapo huku risasi iliyomuua mama huyo ikiingia kichwani mwa Satrine na kukwama kwenye ubongo wake.

Satrine alipelekwa Nairobi kwa matibabu maalum kutoka Mombasa kutokana na ukosefu wa wataalamu wa upasuaji wa ubongo mjini humo.

Shughuli ya kuondoa risasi hiyo ilichukua saa tatu na ilifanywa na madaktari watatu wakiongozwa Daktari Mwangi Gichuru ambaye ni mkuu wa kitengo cha upasuaji wa neva katika hospitali hiyo.

Matoto Satrine yuko salama na daktari Mwangi anasema hawakupata matatizo walipokuwa wanafanya upasuaji huo.

No comments:

Post a Comment