Wednesday 23 April 2014

'Tattoo' yamtia mashakani mtalii Sri Lanka

Tatoo ya Naomi Michelle Coleman inaonyesha picha ya Budhaa ambaye ni Mungu waumini wa dini ya Budhaa.

Mtalii mmoja muingereza amekataliwa kuingia nchini Sri Lanka baada ya kupatikana akiwa amechorwa 'Tattoo' ya Budhaa kwenye mkono wake.
Naomi Michelle Coleman, alikamatwa na maafisa wakuu alipowasili katika uwanja wa ndege katika mji mkuu Colombo baada ya maafisa wakuu kuiona 'Tattoo' hiyo kwenye mkono wake wa kulia.
Budhaa alikuwa mtu mwenye busara na hekima kubwa na pia mwanzilishi wa dini hiyo ambayo mafunzo yake mengi yalijenga msingi wa dini yenyewe.
Msemaji wa polisi alisema kuwa mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 37, alikamatwa kwa kosa la kuwachukiza watu wa dini ya Budhaa na pia kwa kuumiza hisia zao za kidini.
Hakimu aliamuru Bi Coleman arejeshwe nchini mwao.
Kwa sasa anazuiliwa katika kituo cha wahamiaji wanaosubiri kurejeshwa makwao.
Maafisa huchukua hatua kali dhidi ya watu wanaonekana kutusi dini ya Budhaa ambayo waumini wake wengi wanatoka kabila la Sinhalese lenye idadi kubwa ya watu nchini humo.
Bi Coleman aliwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Bandaranaike siku ya Jumatatu kutoka nchini India ambapo maafisa punde ya kuiona Tattoo hiyo ya Budhaa akiwa amekaa kwenye mauwa, walimkamata.
Mwezi Machi mtalii mwingine muingereza, alizuiwa kuingia katika uwanja huo baada ya maafisa kusema kuwa alijibu kijeuri alipohojiwa kuhusu Tattoo aliyokuwa amechorwa ambayo pia ilikuwa na Budhaa.
Bi Coleman anazuiliwa katika kituo cha wahamiaji wanaosubiri kurejeshwa makwao

Maafisa wa Sri Lanka ni wakali sana kwa watu wanaoonekana kudhihaki dini ya Budha

No comments:

Post a Comment