Sunday 29 September 2013

BABU WA KIKOMBE LOLIONDO AIBUKA

Mchungaji Ambilikile Mwaisapila (Babu wa Kikombe) wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), amesema Mungu ameendelea kujifunua kwake na kumuonesha kuwa Tanzania itakuwa kioo cha Afrika na dunia kwa ujumla.

Alitoa kauli hiyo juzi mbele ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakati akizungumza na wakazi wa kijiji cha Samunge, wilayani Ngorongoro mkoani Arusha wakati msafara wa Waziri Mkuu uliposimama nyumbani kwake ili kumsalimia akiwa njiani kurejea mjini Arusha.
Mchungaji Mstaafu Mwaisapila alisema kuna mambo mengi ambayo yameandikwa kwenye Biblia, lakini hayakutokea Israeli na sasa yatafanyika hapa Samunge.
“Mungu ametupenda sana, yanakuja mambo makubwa na wala hayako mbali. Kama mimi ni mzee na nitayaona, kwa hiyo mtarajie kuwa hayako mbali kutokea,” alisema huku akishangiliwa na wananchi.
Alisema katika mafunuo aliyopewa na Mungu ameoneshwa kwamba watu wengi zaidi watafurika kijijini Samunge kuliko ilivyokuwa hapo awali. Alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kwa misaada iliyotoa wakati wa kugawa kikombe ikiwemo mahema, maji na ulinzi.
Waziri Mkuu, Pinda ambaye yuko mkoani Arusha kwa ziara maalum ya kusikiliza matatizo na migogoro ya ardhi yanayowakabili wakazi wa wilaya ya Ngorongoro, katika tarafa za Ngorongoro, Loliondo na Sale alisema anakubaliana na utabiri wa Mch. Mwaisapila kwani Tanzania imejaliwa gesi nyingi na mafuta mengi ambavyo vitabadili sura ya Taifa hili.
"Mungu ametupa gesi nyingi sana, katika miaka miwili tutakuwa na umeme kila mahali. Tuna makaa ya mawe ambayo ni nishati kubwa na sasa tuna fursa ya kupata nishati ya umeme kutoka ardhini (Geo-thermal) katika Ziwa Natron," alisema.
Alisema Tanzania imekuwa kimbilio la kila mwekezaji na sababu kubwa ni amani na utulivu uliopo nchini. Aliwaeleza wakazi wa Samunge kwamba mapema mwakani mkandarasi wa barabara atakuwa katika eneo lao kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya lami ambapo awamu ya kwanza itaanzia Wasso hadi Mto wa Mbu kupitia Samunge.

No comments:

Post a Comment