Sunday 29 September 2013

Kiama cha wauza unga chaja, faini kuondolewa, kifungo ni cha maisha


Serikali imependekeza marekebisho ya sheria ya kudhibiti dawa za kulevya itakayotoa hukumu ya kifungo cha maisha na kufuta kipengele kwenye sheria ya sasa kinachompa mshtakiwa nafasi ya kulipa faini.
Sheria iliyopo sasa ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya ya mwaka 1995 (Sura ya 95, Ibara ya 16) inasema, endapo mtu atakamatwa kwa kosa la kumiliki, kusafirisha, kuzalisha au kutengeneza mashine ya dawa za kulevya, atahukumiwa kifungo cha maisha jela au kulipa faini ya Sh10 milioni.
Hatua hiyo inakuja wakati idadi ya Watanzania wanaosafirisha, kuzalisha na kutumia dawa hizo ikiongezeka hapa nchini.
Pamoja na mapendekezo hayo, wadau mbalimbali wamesema kufanyika kwa maboresho hayo hakutasaidia kupambana na tatizo lililopo hivi sasa, ikiwa maadili ya wananchi na viongozi yaliyoporomoka hayatarekebishwa.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Kitila Mkumbo alisema sheria yoyote itakayowekwa haiwezi kuwa ‘mwarobaini’ wa kutibu tatizo la dawa za kulevya hapa nchini kama wanaohusika hawatawajibishwa.
“Hivi sasa zipo sheria, lakini hazitekelezwi. Kuna baadhi ya viongozi wakubwa kabisa wametajwa kujihusisha na dawa za kulevya, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa,” alisema Mkumbo.
Mbunge wa Kawe na Mjumbe wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ya Bunge, Halima Mdee, alisema Tanzania ina sheria nzuri na bora, lakini changamoto ipo katika utekelezaji wake kwa kuwa rushwa ina mchango mkubwa katika kudhoofisha maendeleo ya taifa.
Mdee alisema ingawa sheria ya rushwa iliyopo hivi sasa ni nzuri, ina kasoro kadhaa zinazohitaji kufanyiwa marekebisho ili kuipa nguvu zaidi.
Alisema baadhi ya viongozi waliopewa dhamana na wananchi wanatuhumiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya.
“Kama mtandao wa dawa za kulevya tunaousikia upo kuanzia viongozi wakubwa hadi wa chini, unadhani hata ukiwa na sheria nzuri itatekelezwa na nani? alihoji Mdee.
Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini, Godfrey Nzowa alisema mapendekezo ya sheria ya dawa za kulevya ni mazuri, lakini yana changamoto nyingi katika utekelezaji wake.

No comments:

Post a Comment