Sunday 29 September 2013

mwanzo Habari Kitaifa Kitaifa Ugaidi Kenya: Kibao chawageukia mawaziri


Nairobi. Shambulizi la kigaidi lililoua watu 67 nchini Kenya wiki iliyopita, limeanza kuchukua sura mpya baada ya kubainika kuwa mawaziri wanne na mkuu wa majeshi walipewa tahadhari kabla kuhusu kutokea kwa tukio hilo.
Taarifa hizo mpya zimekuja wakati ripoti nyingine za uchunguzi zikibainisha kuwa huenda magaidi walioshambulia jengo la Westgate walitoroka kupitia njia ya ardhini inayoanzia kwenye maegesho ya magari chini ya jengo hilo.
Kuhusu mawaziri
Tahadhari hiyo iliyoanza kutolewa Januari mwaka huu, iliwaonya viongozi hao ambao pia ni wanachama wa Baraza la Usalama la Taifa, kuwa Kundi la Al-Shabaab lilikuwa likipanga shambulizi jijini Nairobi.
Kwa mujibu wa ripoti ya kuzuia ugaidi iliyonukuliwa na Gazeti la The Saturday Nation, imewataja Waziri wa Fedha, Julius Rotich, Waziri wa Mambo ya Ndani, Joseph ole Lenku, Waziri wa Ulinzi, Raychelle Omamo, Waziri wa Mambo ya Nje, Amina Mohammed na Mkuu wa Majeshi, Jenerali Julius Karangi kuwa walikuwa na taarifa za shambulizi hilo.
“Taarifa ilitolewa kwao ikiwatahadharisha kuongezeka kwa vitisho vya ugaidi na mipango ya kuanzishwa kwa mashambulizi mfululizo katika miji ya Nairobi na Mombasa kati ya Septemba 13 na 20, 2013,” inasema ripoti hiyo.
Ripoti hiyo inasema kuwa magaidi walikuwa wakipanga shambulizi linalofanana na lile lililotokea Mumbai, India ambapo walishambulia jengo na kuteka raia.
Pia, taarifa hiyo ilitolewa kwa Kamati ya Ushauri ya Usalama wa Taifa katikati ya Septemba, mwaka huu ambapo taarifa za kiintelijensia zilionyesha kuwa Al-Shabaab wameongeza harakati zao Kenya na kwamba walikuwa wanapanga shambulizi.
Kamati hiyo ambayo ndiyo ngazi ya juu ya usalama nchini Kenya, inajumuisha Rais, Naibu Rais, Waziri wa Ulinzi, Mambo ya Nje, Mambo ya Ndani, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mkuu wa Majeshi, Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa na Mkuu wa Jeshi la Polisi.
Viongozi wote waliotajwa kupewa taarifa hawakupatikana, hata ujumbe mfupi wa maandishi waliotumiwa na gazeti hilo kwenye simu zao haukujibiwa.
Shambulizi la wiki iliyopita kwenye jengo la kibiashara la Westgate jijini Nairobi, linalomilikiwa wa raia wa Israel, liliua watu 67 na zaidi ya watu 170 kujeruhiwa.

No comments:

Post a Comment