Monday 27 January 2014

Wazazi wa Bale bado waishi kimaskini



LICHA ya umilionea wake mkubwa unaoongezeka kila kukicha kutokana na mafanikio yake makubwa katika soka, wazazi wa staa wa Real Madrid, Gareth Bale wameendelea kuishi katika nyumba yao ya kimaskini jijini Cardiff.
Si kwa sababu ya tabia za uchoyo za staa huyo, hapana, Bale si mchoyo, lakini wazazi wake wenyewe wamemkatalia kuhamia katika nyumba ya kifahari aliyowanunulia kwa sababu wanapenda kuendelea kukaa katika nyumba ya kota.
Bale, ambaye ni mwanasoka ghali zaidi duniani baada ya kuhamishwa kwa kiasi cha Pauni 85 milioni kutoka Tottenham Hotspur kwenda Real Madrid katika usajili wa kipindi cha majira ya joto cha mwaka jana alisema angewapatia wazazi wake, Frank na Debbie kiasi cha Pauni 1 milioni kwa ajili ya kutafuta jumba la kifahari la kununua na kutimiza ndoto zao za kuishi maisha mazuri.
Lakini wazazi hao walimwambia Bale (24), kwamba wamezoea na kusikia raha kuishi katika nyumba yao ya vyumba vitatu ambayo Bale alikulia kabla ya kuibuka kuwa mchezaji ghali duniani.
Debbie (50), alimwambia rafiki wa familia yake hiyo kwamba kitendo cha Gareth kuwapa ofa ya nyumba kilikuwa cha huruma na kizuri, lakini wanapenda kuendelea kuishi walipo huku wakiwa na majirani wazuri waliowazoea.
Yeye na mumewe, Frank (54),  ambaye ni mstaafu wa shule moja jijini humo, walinunua nyumba hiyo ya kawaida kwa kiasi cha Pauni 12,000 miaka 30 iliyopita kabla ya Bale hajazaliwa na kwa sasa nyumbani hiyo ina thamani ya Pauni 170,000.
Ni hapo ndipo walipomlea Bale na dada yake, Vicky huku Bale akijifunza kucheza soka katika bustani iliyopo kando ya nyumba hiyo na kuharibu mali za watu.
Baada ya kupatiwa kiasi hicho cha pesa na Bale kwa ajili ya kusaka nyumba, yeye na mumewe walienda kutafuta nyumba ya kifahari katika eneo la Vale of Glamorgan. Vile vile walitafuta nyumba yenye thamani ya Pauni 415,000 karibu na eneo la wanaloishi.
Hata hivyo, mwishowe waliamua moja kwa moja kubaki katika nyumba yao waliyoishi kwa miaka 30 iliyopita ambayo inaashiria historia yao huku wakigoma kuwaacha majirani zao wenye upendo wa dhati kwao.
Debbie alimwambia rafiki yake mmoja kuwa wanapata kila wanachokitaka kwa kuwa hapo na itakuwa jambo gumu kwao kuhama katika nyumba ambayo watoto wao walikulia.

No comments:

Post a Comment