Tuesday 4 February 2014

ANAYEDAIWA KUZAA NA MWINGIRA AZUA MAPYA


KESI ya Nabii na Mtume Josephat Elias Mwingira wa Kanisa la Efhata, kudaiwa kuzaa na mke wa Dk. William Morris, Dk. Phillis Nyambi inaendelea kuunguruma katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar ambapo mlalamikiwa huyo wa pili katika shauri hilo amekiri kuzaa nje ya ndoa.
Dk. Philis Nyimbi anayedaiwa kuzaa na Nabii Mwingira.
Mlalamikiwa huyo, Dk. Phillis Morris Nyambi katika majibu yake ya kimaandishi yaliyotolewa Januari 22, mwaka huu mahakamani hapo (nakala tunayo), amekiri kuzaa na mtu ambaye alisema hamfahamu wala hajui alipo!!
Mwanamke huyo ambaye kitaaluma ni daktari kama alivyo mumewe, raia wa Liberia, amekana kuzaa na Nabii Mwingira.
ATOA SABABU ZA KUZAA NJE YA NDOA
Wakili Mbogoro anayemwakilisha mahakamani Dk. Phillis alisema mteja wake yalimpata ya kuzaa nje ya ndoa baada ya mlalamikaji (mume) kumtelekeza kwa miaka saba, kuanzia 2002-2009.
“Mlalamikiwa wa pili akiwa ni binadamu akajikuta akishindwa majaribu,” alisema wakili huyo katika majibu hayo.
Kiongozi wa Kanisa la Efatha, Nabii Josephat Mwingira, anyetuhumiwa kuzaa na mke wa mtu.
Aliongeza kuwa mlalamikaji alielezwa hali halisi na akamhakikishia mlalamikiwa mbele ya wazee kwamba anapaswa kulaumiwa na atamtunza mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa kama wake.
Hata hivyo, mke huyo aliiambia mahakama kuwa kila mtu ajiulize kwa nini mlalamikaji amekuja juu kuhusiana na mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa na sababu gani hajachukua hatua yoyote baada ya miaka mitatu tangu azaliwe (2009 hadi 2012) licha ya kudaiwa kuwa shauri hilo lilifikishwa polisi.
OMBI LA KUPIMWA UKIMWI
Kuhusu ombi la mlalamikaji kuitaka mahakama iamuru walalamikiwa Nabii Mwingira na Dk. Phillis kupimwa Virusi vya Ukimwi, Wakili Mbogoro amelipinga kwa madai ya kesi kupitwa na wakati.
Akifunga utetezi wake, Mbogoro ameitaka mahakama kuitupilia mbali kesi hiyo na mlalamikaji kulipa gharama.
Dk. Morris anayewakilishwa na Wakili Desidery Ndibalema amemshitaki Nabii Mwingira kama mlalamikiwa namba moja na mke wake mlalamikaji, Dk. Phillis ni mlalamikiwa wa pili na tayari shauri hilo lililopelekwa mahakamani Novemba 21, mwaka jana limepewa jalada lenye usajili namba 306 la 2013 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar.
Mtoto anayedaiwa kuwa wa Nabii Mwingira aliyezaa na Dk. Philis.
Mlalamikaji amedai kuwa wawili hao wamemvurugia ndoa yake baada ya kujiingiza katika uhusiano wa kimapenzi na kuzaa mtoto mmoja.
Kutokana na mambo hayo, ameiomba mahakama iwaamuru walalamikiwa hao wamlipe fidia ya shilingi bilioni 7.5.
Dk.  Morris alifunga ndoa na Dk. Phillis Desemba 28, 2001 katika Kanisa la Saint Albano, Upanga jijini Dar.
MWINGIRA KIMYA
Mpaka mahakama inaahirisha kesi hiyo, Nabii Mwingira hakuwa amewasilisha utetezi wake na shauri hilo limepangwa kusikilizwa tena Februari 22, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment