Tuesday 25 February 2014

Tiketi zinatia najisi soka la Tanzania

MWAKA mpya 2014 ulianza kwa matumaini makubwa miongoni mwa wadau wa soka kwamba maendeleo yamefikiwa, ambapo ilitarajiwa Tanzania ianze kutumia tiketi za elektroniki.
Tiketi hizo zilianza kutumika lakini yalikuwa majanga, teknolojia ikakataa au wadau wakashindwa kuiweka inavyotakiwa.
Sintofahamu hiyo imeturudisha kule kule kwenye tiketi za vishina, ambapo kuna wanaofaidi kwa kukaa milangoni.
Nimeambiwa kuna jamaa wana vishina vya mechi zilizopita baina ya Yanga na Al Ahly na kwamba si ajabu hata mechi ijayo watavitumia au kurekebisha kidogo tu.
Soka imekuwa sehemu ya kwenda kula na si sehemu ya kwenda kutumia uzalendo, elimu, ujuzi na maarifa kuhakikisha sekta hii nayo inakua kiteknolojia na kulifaidisha taifa kiuchumi.
Tiketi za elektroniki ni hatua moja ndogo tu ya kuendea usasa zaidi, kwa sababu wenzetu huku wanabofya kwenye mtandao wa kompyuta, kulipia na kupata tiketi. Tutaona baadaye mifumo yao, manufaa na mapungufu kama yapo.
Kwetu Tanga yalikuwa maafa zaidi maana milango ya elektroniki haikuwafungulia washabiki waliofika Mkwakwani na inaelezwa zaidi ya nusu ya washabiki waliingia bure.
Wapo watu hata ndani ya mfumo wa uongozi wa soka katika klabu, mikoa na ngazi ya taifa wanapendelea mfumo wa kuchana tiketi pale mlangoni.
Ndiyo maana nachelea kusema kwamba mfuko wa elektroniki umekwama bali labda itakuwa sahihi zaidi kusema umekwamishwa.
Zipo tetesi pia kwamba Wachina walipokuwa wakijenga Uwanja wa Taifa ambao ni wa kisasa zaidi Afrika Mashariki walitoa wazo la kuweka mfumo huo moja kwa moja lakini ‘wadau wa maendeleo’ wakakataa. Kisa? Wanajua wao.
Kwa hali ilivyokuwa mbaya, wakati Ligi Kuu Tanzania inaanza kuhusiana na suala la tiketi, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) halikuwa na la kufanya zaidi ya kuzuia matumizi ya tiketi hizo. Niseme tu kwamba kuna watu waliopinga tangu awali tiketi hizo na wataendelea kupinga nyingine zozote zenye mfumo wa kuziba mianya ya wizi.
Wenzetu hapa Uingereza na mataifa mengine yaliyoendelea kisoka, ambayo hatuna budi kuyaiga katika mazuri yao, wanaoruhusiwa kuuza tiketi za mechi hapa ni klabu husika tu au mawakala wao waliopo kisheria na si kuchagua sijui vibanda vya soda au mikate Mwenge, Tandika au Ilala Bungoni.
Ni kosa kubwa kujihusisha na uuzaji wa tiketi ovyo, lakini kama ambavyo kuna wachumia tumbo hapo nyumbani, wapo hapa wanaojaribu kuzi upload tiketi kwenye tovuti mbalimbali na baadhi hudiriki kwenda karibu na viwanja na kuziuza kwa bei ya juu.
Bodi ya Ligi Kuu (Premier League) hapa England wamekuwa wakali sana wakishirikiana na mamlaka za dola kupambana kwa mafanikio makubwa na wauzaji feki wanaotundika tiketi kwenye tovuti na kuziuza na pia watu kadhaa wamedakwa na kushitakiwa kwa kuzilangua viwanjani.
Hili, pengine sawa na linaloweza kuwa limetokea au litatokea nyumbani, linakwenda sambamba na uuzaji wa tiketi za kughushi, ndiyo maana kama kuna kitu kinasisitizwa sana kwenye nchi hizi ni kununua tiketi (na bidhaa nyingine zozote) kwa mhusika halali na kupata stakabadhi.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inaposisitiza ukinunua dai stakabadhi na ukiuza toa stakabadhi, ni jambo ambalo huku ni la lazima, hata kama hutaki utajikuta umechanganyiwa stakabadhi ama na bidhaa zako au na chenji.
Klabu mwenyeji huuza tiketi zake lakini huwawekea wageni idadi wanayokubaliana na hutolewa mapema, iwe ni mechi ya Ligi Kuu au ya kimataifa na wala hutaona mkanganyiko.
Tiketi zikisemwa zimeisha basi shabiki ambaye angetaka kwenda uwanjani anashauriwa abaki nyumbani, atazame kwenye televisheni na kuwahi kutazama mtandaoni ratiba ya mechi inayofuata anunue mapema tiketi yake awe nayo kibindoni.
Malalamiko ambayo yamepata kuwapo ni tiketi za baadhi ya mechi kuwa ghali sana, mojawapo ya klabu zenye aina hiyo ni Arsenal lakini watu wanaoingia Emirates ni karibu 60,000.
Bodi ya EPL kwa mfano, imekuwa ikisambaza matangazo kwa njia mbalimbali kuwaasa washabiki walio ng’ambo ambao wangependa kuingia England kutazama mechi za EPL kuwasiliana kwanza na klabu husika kwenye tovuti zao.
Ni tofauti kabisa na jamaa wa Mbeya City wanaopanda Coaster zao na kutinga Dar kwa ajili ya mechi dhidi ya Simba siku hiyo hiyo ya mechi pasipo kuwa na tiketi mkononi, maana watazipata tu uwanjani na wanasema uwanja haujai, kwani eti si sawa na ndoo ya maji.
Premier League pia inatoa angalizo kwa washabiki hao, hasa wa ng’ambo kupendelea zaidi kununua tiketi kutoka kwa klabu husika ili kujiridhisha kwamba ni halali.
Ununuzi wote huo ni kwa mtandao, ambao rafiki zangu wa Tanzania watakuwa hawaupendi.
Tiketi za mechi za EPL zina soko sana kutokana na washabiki wengi kupenda kwenda wenyewe uwanjani kujionea mechi na wachezaji wawapendao, hata kwa kusafiri umbali mrefu.


I.G.Saria,
M: +44 (0) 7791284317
E: saria@tanzaniasports.com

No comments:

Post a Comment