Monday 3 February 2014

Yanga yaitungua Mbeya City, Azam yafanya kufuru


TANGU kuanza kwa Ligi Kuu Bara msimu wa 2013/14 kuna wanaume wawili tu waliokuwa hawajapoteza mechi yoyote kwenye Ligi.
Wanaume hao ni Azam Fc na Mbeya City, lakini mambo yamebadilika. Kwa mara ya kwanza Mbeya City imepoteza mechi baada ya kukubali kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Yanga jana Jumapili jioni kwenye Uwanja wa Taifa.
Mechi ambayo iliwaweka kwenye wakati mgumu wachezaji wa Mbeya City iliyokuwa na sapoti kubwa ya Simba kwani baada ya mchezo huo wachezaji na mashabiki wa Yanga walikuwa wakiwaonyesha ishara za vidole wakimaanisha “kaeni kimyaa hii ndiyo Yanga Afrika”.
Ushindi wa Yanga umeipa pointi 35 ikatulia kwenye nafasi ya pili, baada ya Azam kuikung’uta bila huruma Kagera Sugar mabao 4-0 kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi. Azam imetimiza pointi 36 huku Mbeya City ikiendelea kushika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi 31 wakati Simba ni ya nne ikiwa na pointi 27.
Yanga walionekana kuishambulia kwa umakini Mbeya City ingawa vijana hao wa Mbeya hawakukata tamaa na walionyesha kujiamini na walicheza kwa nguvu jambo ambalo mara kadhaa liliwatisha Yanga.
Sekunde la 48, Simon Msuva alipoteza nafasi ya wazi baada ya kupiga shuti lililopaa juu akipokea pasi ya Oscar Joshua wakati wapinzani wao Mbeya City nao wakikosa bao la wazi dakika 13 baada ya mchezaji wao Paul Nonga kupiga shuti ndefu na mpira kutoka nje akitumia makosa ya Kelvin Yondani.
Mrisho Ngassa wa Yanga alifunga bao pekee na la ushindi kwenye mchezo huo dakika 16, akipiga shuti kuunganisha mpira wa kichwa uliopigwa na beki wa Mbeya City, Yusuf Abdallah aliyekuwa akiokoa krosi safi ya David Luhende.
Yanga walionekana kulishambulia kwa nguvu lango la Mbeya City huku Mwagane Yeya akipoteza nafasi dakika 24 baada ya kupiga mpira kwa kichwa na kushindwa kulenga lango akipokea krosi ya Kaseke.
Luhende alipoteza nafasi ya wazi dakika 27 baada ya kupiga shuti ndefu na mpira kutoka nje akipokea pasi safi ya Didier Kavumbagu, dakika 31 kipa wa Yanga Deo Munishi ‘Dida’ aliokoa hatari iliyotokana na krosi ya Peter Mapunda iliyokuwa ikisubiriwa na Yeya tayari kwa kufunga.
Bahati haikuwa ya Nonga kwani dakika 35 pia alipoteza nafasi ya kuipatia bao timu yake baada ya shuti lake kupanguliwa na Dida huku dakika ya 41 Nonga akiinyima tena timu yake bao la wazi kwani shuti lake lilitoka nje kidogo baada ya kupokea pasi safi ya Mapunda aliyemkimbiza vibaya Oscar Joshua winga ya kulia.
Kipindi cha pili Mbeya City ilipata pigo baada ya kiungo wake Mazanda kupewa kadi nyekundu baada ya kutoka kwenye mstari kabla ya mpira kupigwa wakati Yanga ikitaka kupiga mpira wa adhabu baada ya Hassan Mwasipili kuunawa mpira na mwamuzi Abdallah Kambuzi kuampa kadi nyekundu.
Dakika 61 Kocha wa Yanga, Hans Van Der Pluijm alifanya mabadiliko, alimtoa Mbuyu Twite na kumuingiza Juma Abdul alimtoa Didier Kavumbagu dakika 64 nafasi yake ilichukuliwa na Hamis Kiiza.

MWANASIPOTI

No comments:

Post a Comment