Monday 3 February 2014

Kikwete aingilia kati vita ya urais CCM

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete ameingilia kati vita ya kuwania urais mwaka 2015 kwa kukemea kwa baadhi ya makada wa chama hicho kuanza kampeni mapema.

Kadhalika, ameziagiza Kamati za Maadili na Usalama za chama hicho kuwachukulia hatua stahiki viongozi na wanachama wake wanaomwaga fedha ili kupata uongozi.
Rais Kikwete alizungumzia masuala hayo kwa nyakati mbili tofauti; juzi wakati alipokutana na Halmashauri ya CCM ya Mkoa wa Mbeya na jana kwenye kilele cha sherehe za maadhimisho ya miaka 37 ya kuzaliwa chama hicho.
Kauli yake imekuja wakati kukiwa na vita ya maneno baina ya makada wa chama hicho, kutokana na kauli iliyotolewa na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa ambaye alitangaza kuanza rasmi kwa safari aliyoiita ya matumaini ya ndoto zake, ambayo amesema itatimiza ndoto za Watanzania kupata elimu bure, majisafi na maendeleo ya uhakika.
Lowassa alitoa kauli hiyo wakati wa hafla ya mwaka mpya aliyowaandalia marafiki na jamaa zake, Januari Mosi, mwaka huu huko Monduli mkoani Arusha.
Tamko hilo lilileta hisia kuwa ametangaza nia ya kugombea urais mwaka 2015 kupitia CCM na kusababisha malumbano baina ya wazee, vijana, viongozi na makada wa chama hicho wakimtuhumu kuwa anakivuruga chama kwa kutangaza nia hiyo kabla ya muda wa kampeni kuanza.
Akizungumza wajumbe wa Halmashauri ya CCM ya Mkoa wa Mbeya kwenye Ukumbi wa CCM, Mbeya, Rais Kikwete alisema kuanza kwa kampeni kabla ya wakati wake ni moja ya mambo yanayosikitisha.
“Hili ni moja ya mambo yanayosikitisha. Lakini suala zima tumelikabidhi kwa Mzee Mangula (Phillip - Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara), ambaye atalisimamia na kulishughulikia,” alisema.
Rais Kikwete alikuwa akijibu swali na Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Mbeya, Godfrey Zambi ambaye alimtaka kufafanua kama kampeni zimeanza ndani ya CCM au bado.
Kumwaga fedha
Akihutubia katika mkutano wa hadhara kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya jana, Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, alisema kutoa fedha kunaharibu taswira ya chama hicho na kukiweka katika hatari ya kupoteza ushindi katika chaguzi zinazokuja.
“Agizo la CCM la miaka mingi iliyopita ni kwamba kila ngazi kuwa na shughuli za kuwaingizia mapato sambamba na kuwa na mfuko wa uchaguzi. Agizo hili bado halijatekelezwa na ndiyo linakiathiri chama,” alisema Rais Kikwete.

Mwananchi

No comments:

Post a Comment