Saturday 14 December 2013

Mapunda ataka namba moja Simba

Kipa mpya wa Simba, Ivo Mapunda amesema hahofii ushindani atakaokutana nao kutoka kwa makipa wengine wa timu hiyo na kudai kuwa yuko tayari kuikabili changamoto hiyo na hatimaye kusimama langoni kama kipa namba moja.
Mapunda alisaini mkataba wa miaka miwili wa kujiunga na klabu ya Simba juzi usiku akitokea Gor Mahia ya Kenya,ikiwa ni saa chache baada ya kuidakia timu ya Taifa ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) katika mechi ya kusaka mshindi wa tatu dhidi ya Zambia kwenye Chalenji.
Ni dhahiri, Mapunda aliyewahi pia kuidakia Yanga atakuwa na kazi ya ziada ya kuthibitisha ubora wake ili aweze kupewa hadhi ya kuwa kipa wa kwanza Simba na kuwabwaga makipa wengine wa timu hiyo ambao ni Yaw Berko kutoka Ghana na Abuu Hashim.
Hata hivyo, Berko ambaye alimwaga wino hivi karibuni kujiunga na Wekundu wa Msimbazi ndiye anaonekana kuwa tishio kwa Mapunda kutokana na rekodi yake nzuri aliyoiandaa wakati akiichezea Yanga. Lakini, kipa huyo kasaini mkataba wa miezi sita tu.
Akizungumza na Mwananchi kwa simu saa chache kabla ya kuondoka Kenya kurejea Tanzania, Mapunda alisema “sina wasiwasi, mimi ni kipa mzoefu na hata Watanzania wanajua uwezo wangu.
“Baada ya kusaini, sasa ni kazi tu, kikubwa naomba ushirikiano na Benchi la Ufundi, uongozi, wachezaji wenzangu na mashabiki na wadau kwa ujumla,” alisema Mapunda.
Klabu zingine alizowahi kuzichezea Mapunda ni Tukuyu Stars na Tanzania Prisons za Mbeya, Moro United (Morogoro) Bandari Mombasa (Kenya) na Saint George ya Ethiopia.
Mapunda pia aliiwezesha Gor Mahia kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Kenya msimu huu ikiwa imepita miaka 18 tangu ilipofanya hivyo kwa mara ya mwisho.
Wakati huohuo; Simba imesisitiza kwamba sasa imemaliza kazi baada ya kupata majembe mawili ya maana na sasa inarudi uwanjani huku beki mpya, Donaldi Mosoti akiahidi kufanya kazi ya uhakika.
Beki huyo amesaini mkataba wa miaka miwili mbele ya mwanasheria na Katibu wa Simba, Evodius Mtawala mjini Nairobi.
Mtawala alisema: “Tumemaliza usajili sasa tunarudi uwanjani kufanya kazi.”Mbali na huyo hata kipa namba moja wa Stars, Ivo Mapunda naye amesaini mkataba wa mwaka mmoja na nusu kuichezea Simba.Mapunda alikuwa kipa tegemeo wa Gor Mahia ya Kenya hasa kwenye penalti sawa na Mosoti ambaye mashabiki wa Gor Mahia hawaamini kwamba ameondoka.Mosoti alisema jana mjini hapa kwamba: “Nimefurahi sana kusaini na Simba, nakwenda kufanya kazi na Loga (Zdavko Logarusic) ambaye nimekaa nae kwa mafanikio Gor Mahia.”
“Nina uzoefu wa kutosha na soka la Afrika Mashariki na ninadhani nitafanya kazi nzuri na Simba kama Wakenya wenzangu waliopita, kikubwa ni ushirikiano tu.”Makamu Mwenyekiti wa Kwanza wa Gor mahia, Faz Ochieng alisisitiza jana kwamba watakaa kujadiliana nini cha kufanya na hajapata taarifa rasmi za kuondoka kwa wachezaji hao lakini akakiri mikataba yao inamalizika mwezi huu.

No comments:

Post a Comment