Wednesday 18 December 2013

Rage ataja waliomuuza Okwi Yanga


MWENYEKITI aliyesimamishwa wa Simba, Ismail Rage, amefanya kikao na baadhi ya wanachama wa timu hiyo na kutoa siri kwamba waliomuuza mshambuliaji Emmanuel Okwi kwa Yanga ni Waganda, SC Villa, lakini akasisitiza ni hujuma kutoka ndani ya klabu hiyo.

Emmanuel Okwi.
Championi Jumatano lilikuwa likipata ‘live’ kila kinachoendelea ndani ya kikao hicho kilichofanyika makao makuu ya klabu ya Simba, barabara ya Msimbazi jijini Dar es Salaam, jana.
Akionyesha mwenye masikitiko, Rage alisema kuna baadhi ya viongozi wa klabu hiyo wanahusika katika usajili wa Okwi aliyetua Yanga kwa mkataba wa miaka miwili na nusu.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Rage.
Rage, amesema Okwi raia wa Uganda, mpaka sasa anakabiliwa na kesi tatu muhimu na kuzitaja ya kwanza ni ile ya nyota huyo kukakabiliwa na mashtaka ya kutoroka katika klabu yake ya zamani ya Etoile du Sahel ya Tunisia (ESS).
Shitaka la pili ni kuhusu SC Villa, ambao walipewa Okwi kwa mkopo lakini wakamuuza Yanga na tatu ni kesi yake aliyoifungua Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) kuhusu ESS, ambapo kabla ya shirikisho hilo kutoa majibu nyota huyo kukubali, Mganda huyo kauzwa Yanga.
“Nilipiga simu Fifa kutaka kujua kujua kuhusu Okwi, nikaambiwa kuna fedha dola 5,900 ambazo ni kwa ajili ya kusikilizwa kwa kesi yetu, mwisho ilikuwa saa nne asubuhi leo (jana). Barua ilishatumwa tangu Desemba 6, lakini hakuna aliyeijibu na wakaificha,” alisema Rage akitaka kudondosha chozi ‘live’.
“Saa tatu asubuhi nikatuma fedha hizo ambazo zitatoa nafasi ya kusikilizwa kwa jambo hilo. Kama ningechelewa, basi Okwi angeweza kuwa mchezaji huru kwenda Yanga,” alisema Rage katika kikao hicho kilichofanyika kuanzia saa 10:15 hadi saa 11:45 jioni.
Aidha, Rage amesema anajua kuwa kamati ya utendaji ya timu hiyo inachangia kumhujumu ili aonekane hafai katika klabu hiyo, ambapo sasa ataitisha mkutano mkuu Januari mwakani.
“Simba imejaa wanafiki, wanafanya mpango wachezaji waende Yanga. Mfano, Okwi alishatangaza anaitaka Simba, vipi hawakumsajili na utaona mambo yanaharibika kila nikiwa nje ya nchi. Pia TFF kuna watu kama hao na wanachangia kutuhujumu na kuniharibia,” alisema.
Kuhusiana na suala la uchaguzi, Rage rasmi ametangaza kwamba hatagombea nafasi hiyo tena na badala yake kuna mtu amemuandaa.
“Tayari nimemuandaa mtu, siwezi kumtaja sasa ila nitawaacha wanachama waamue utakapofika uchaguzi,” alisema Rage.
Mzigo wa Okwi umekuwa ukimuangukia Rage kwa kuwa ndiye alifunga safari kwenda kumuuza Tunisia, lakini akarejea mikono mitupu na dola 300,000 za mauzo zikabaki Tunisia na hadi leo ni hadithi.

GPL

No comments:

Post a Comment