Tuesday 17 December 2013

Ndoa ya Yanga na Okwi katika nyuma ya pazia, sinema ndio kwanza imeanza


AFANDE Sele, mwanamuziki maarufu wa kizazi kipya nchini, aliwahi kuimba katika wimbo wake fulani hivi akisema; ‘Aliwazalo mjinga ndilo litakalomtokea.’
Leo, miaka kadhaa baada ya mstari ule, Yanga kimewatokea walichokuwa wanawaza kwa muda mrefu, lakini wakaonekana wajinga.
Tangu Emmanuel Okwi apate makali katika miguu yake miaka minne iliyopita Mtaa wa Msimbazi, jijini Dar es Salaam, Yanga walikuwa wanawaza kumpata, na kweli wamempata.
Maswali mengi kuliko majibu
Kabla Okwi hajavaa jezi za njano na kijani, kuna maswali mengi yanayopaswa kujibiwa ingawa majibu yake hayaonekani hewani. Tatizo si Yanga imempataje Okwi. Tunajua kuwa fitina maridadi za usajili kwa sasa zimehamia Yanga baada ya kufifia kwa kundi la Friends of Simba la klabu ya Simba ambao ndio walikuwa hodari zaidi kwa fitina hizi kabla ya kuibuka kwa watu wanaoitwa akina Bin Kleb, Seif Magari, Mussa Katabaro na wengineo pale Jangwani.
Lakini maswali yanakuja. Ni kweli Simba haijalipwa pesa za Okwi? Kama wamelipwa, nani alipokea? Kwa nini SC Villa wameruhusiwa kumuuza mchezaji ambaye alitajwa kuwa yupo kwa mkopo tu klabuni kwao kwa ruhusa maalumu kutoka Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa)?
Nani hasa alikuwa anammiliki Okwi kati ya SC Villa ya Uganda na Etoile du Sahel ya Tunisia? Lakini pia kwa sasa kuna mfumo wa Transfer Matching System (TMS) ambapo jina la mchezaji mwenye matatizo lisingeweza kukubali kuingia katika orodha ya wachezaji wa Yanga. Mbona Yanga wamefanikiwa kuliingiza jina la Okwi? Kwa nini wamepata ITC kama kweli Okwi alikuwa ana matatizo?
Kitanzi katika shingo ya Simba
Alfajiri ambayo kiungo Patrick Mafisango alifariki, ilidaiwa kwamba dakika chache kabla hajakutana na ajali alikuwa anakwepa kusaini mkataba mpya na klabu ya Simba huku viongozi wao wakidaiwa kutembea na dola kadhaa za kumpa Mcongo huyo.
Hata hivyo, inadaiwa kuwa Mafisango alikuwa na mpango wa kwenda kucheza nje ya nchi, au kusaini Yanga. Kama kweli angesaini Yanga, leo Yanga ingekuwa na wachezaji wanne muhimu zaidi katika kikosi cha Simba kilichotamba miaka mitatu iliyopita wakiunda ‘uti wa mgongo’ wa timu.
Ili timu iwe imara inahitaji kuwa na wachezaji wanne ambao ukiwapanga uwanjani unapata ‘uti wa mgongo’, yaani kipa, beki wa kati, kiungo na mshambuliaji.
Kikosi hicho kiliundwa kwa msingi wa kipa, Juma Kaseja, katika ulinzi, nguzo alikuwa Kelvin Yondani, katika kiungo msingi alikuwa Mafisango, katika ushambuliaji nguzo alikuwa Okwi.

Mwanaspoti

No comments:

Post a Comment