Friday 22 November 2013

ELIMU:MAUMIVU YA KIFUA (ANGINA PECTORIS)

Maumivu haya zaidi uhusisha moyo na yanapomtokea mtu huchukua muda mfupi na huisha, aina hii ya maumivu kwa lugha nyingine ya kitaalamu huitwa Kilio cha moyo ambapo misuli ya moyo inayowezesha moyo usukume damu inakosa hewa ya oksijeni hivyo inachoka na kufanya kazi kwa kujilazimisha ndiyo maana hali ikizidi kuwa mbaya utajikunja inakulazimu upumzike au ukae chini.
Chanzo cha tatizo
Maumivu haya ya kifua kama tulivyoona hutokana na misuli ya moyo kufanya kazi huku ikikosa hewa ya oksijeni. Kwenye misuli ya moyo kuna  mishipa ya damu inayosambaza damu katika misuli hiyo.
Mishipa hiyo inayoitwa Coronary Artery. Mishipa hii ni midogo kwa hiyo huwa inaziba kutokana na mafuta mengi kuzunguka kwenye damu au ‘Cholesterol’ au kwa Kiswahili ‘lehemu.’ Mafuta haya huganda  ndani ya mishipa ya damu hivyo hupunguza kipenyo cha mshipa wa damu au bomba la kupitisha damu na mwishowe kuziba kabisa. Mishipa hii ikiziba katika upande mmoja wa moyo husababisha upande huo kitofanya kazi vizuri.
Mahitaji ya mzunguko wa oksijeni katika misuli ya moyo huwa makubwa pale unapojishughulisha kwa mazoezi, aidha kukimbia, kutembea harakaharaka au kupanda ngazi au mlima, hapo utajisikia pumzi inapungua na kifua kinauma.
Maumivu ya kifua zaidi huwa upande wa kushoto na wakati mwingine yakielekea mgongoni upande huohuo.
Jinsi tatizo linavyotokea
Kama tulivyoelezea jinsi maumivu yanavyotokea, mgonjwa atagundua kwamba anatatizo hili la Angina endapo siku zote anaishi vizuri tu, hana presha ya kupanda wala kushuka lakini si mtu wa kufanya mazoezi lakini akijishughulisha kwa mazoezi au kupanda ngazi anapata shida hasa kupanda mlima.
Maumivu anayoyapata katika upande huo wa kifua huwa kama vichomi ambapo kitaalamu tunasema ‘constricting, squeezing or choking’ anajihisi kama  ametiwishwa zigo zito kifuani kwake lakini akikaa na kupumzika  yanaacha.
Maumivu haya yana tabia ya kusambaa endapo yatakuwa makali au utakuwa unayavumilia, husambaa upande wa kifua kushoto kuelekea mgongoni na katikati ya kifua na kuhisi kama unakiungulia yaani moto mkali ndani ya kifua.
Mgonjwa pia anaweza kuhisi maumivu katika bega la kushoto au mabega yote.
 Kwahiyo hata ukiwa umekaa tu utahisi mabega yanauma na kifua kinauma katikati na kusambaa hadi mgongoni na mwili kuwa mchovu. Hali ikiwa mbaya maumivu husambaa hadi shingoni na kwenye mataya na kujihisi kila wakati wewe ni mgonjwa na kuhangaika mara upime malaria, Typhoid au uende kwenye masaji.
Hali hii ya uchovu wa mwili na kujihisi mgonjwa kila wakati husababishwa na misuli ya moyo kutopata oksijeni ya kutosha na mara myingi vipimo vingi utakavyofanyiwa utaambiwa huna tatizo lakini wewe bado unaumwa.
Hali hii huongezeka au huendelea hivyo siku hadi siku endapo akili yako itakuwa na msongo wa mawazo.
Maumivu ya kifua na mwili wakati mwingne huwa makali baada ya tendo la  ndoa.
Maumivu makali na uchovu hupungua dakika ishirini baada ya kujitokeza, unatakiwa upate muda wa kupunguza na  kama ulikuwa unafanya mazoezi uache hadi uonane na daktari wako wa uchunguzi na ushauri.

Uchunguzi
Utafanyika katika hospitali za mikoa, vipimo mbalimbali vinavyohusu moyo hufanyika, historia ya tatizo itachukuliwa kwa undani. Chunguza ulaji na unywaji wako na maisha unayoishi.

Athari za tatizo
Tatizo hili linaweza kukusababishia matatizo makubwa ya moyo ambapo upande mmoja wa moyo unaweza kufa au ‘myocardial infaretion’ endapo tatizo litaendelea kwa muda mrefu, vilevile unaweza kukutwa na mauti ghafla kwa shinikizo au mshtuko wa moyo.
‘Heart Attack. Magonjwa haya tutakuja kuyaona hapo baadaye. Tatizo huathiri nguvu za kiume na  kukosesha hamu ya tendo la ndoa.

Ushauri
Endapo unafanya mazoezi halafu unashindwa kutokana na dalili tulizozielezea au unatembea kwa kupandisha kilima au ngazi inakuwa tabu, basi usidharau muone haraka daktari wako kwa uchunguzi. Pia hata ukiona kabla na wakati wa tendo la ndoa unahisi moyo unaenda mbio basi wahi hospitali. Epuka unywaji pombe, ulaji wa vyakula vyenye mafuta na uvutaji wa sigara,
Pendelea kufanya mazoezi, Tatizo ni kubwa  kwa wasiofanya mazoezi, tumia hata nusu saa kwa siku.

GPL

No comments:

Post a Comment