Wednesday 13 November 2013

TFF yamtimua Dhaira Tanzania

SIMBA imepata taarifa mbaya katika kikosi chao, baada ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kutangaza rasmi kwamba hakuna klabu itakayoruhusiwa kuwa na kipa wa kigeni msimu ujao.
Zakaria Hans Pope ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, ameliambia Championi Jumatano kuwa tayari klabu yake imepokea taarifa hizo kutoka TFF ambapo imezitaka klabu zote kupunguza nyota wao wa Kimataifa kufikia idadi ya wachezaji watatu huku pia kila timu ikitakiwa kuwa na makipa wazawa pekee.
Hans Pope amesema kufuatia taarifa hizo tayari klabu yake imeanza mipango ya kutaka kumuuza Dhaira ili kujiandaa na hilo huku klabu hiyo ikipiga hesabu za kuanza kumvizia kipa Ally Mustapha ‘Barthez’ aliyeko Yanga ambaye mkataba wake umebakiza miezi sita kumalizika.
“Tunalazimika kumuuza Dhaira inawezekana hilo likafanyika katika dirisha hili dogo la usajili au hata mwisho wa msimu, lakini sasa tunaanza maandalizi ya kutafuta mrithi wake ingawa katika timu yetu bado tuna makipa kama yule kijana Abuu, (Hashim) ambaye yuko kwenye kiwango kizuri,” alisema Hans Pope huku akiongeza kwa kusema:
“Bado hatujaanza huo mpango rasmi lakini ni vyema tukaaanza harakati taratibu, hata huyo Barthez unayemtaja kama tukikubaliana tunaweza kumrudisha lakini itategemea kama tutapata timu itakayoweza kumnunua Dhaira kwanza kwa kuwa ni lazima tumuondoshe na tunaamini tutamuuza nje, lakini pia naona kuna ugumu hata wa kusajili nyota mwingine yeyote wa Kimataifa msimu huu.”

Champion

No comments:

Post a Comment