Monday 11 November 2013

Makamba: Ningekuwa Manji ningejiuzulu


NAIBU Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba amemshauri Mwenyekiti wa Yanga, Yusuph Manji kuachana na wadhifa huo na kugeukia ukurugenzi wa soka la vijana.
Makamba, ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye halfa ya utoaji Tuzo ya Mwanasoka Bora wa Tanzania 2012/13 iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam Ijumaa iliyopita alisema kuwa soka la Tanzania haliwezi kufika mbali bila kuwapo na utaratibu mzuri wa kuwekeza kwenye soka la vijana kuanzia miaka tisa.
“Naamini hii ndiyo sehemu ambayo tunakosea, kwa maana hiyo kama ningekuwa Manji (Yusuph) basi ningeachana na uenyekiti na kuomba ukurugenzi wa timu ya vijana, ifike mahali kuwe na utaratibu kwa kila klabu inayoshiriki Ligi Kuu kuwa na akademi yake, tofauti na hapo nafikiri tutaishia kupiga kelele pasipo mabadiliko yoyote,” alisema.
Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli aliipongeza klabu ya Azam kwa jitihada zake za kuanzisha Akademi kwa ajili ya kulea na kukuza vipaji vya soka la vijana.
“Azam wameonyesha hilo, nawapongeza na iwe mfano kwa klabu nyingine kukomboa soka letu,” alisema.
Makamba pia aliimwagia sifa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) ambayo inachapisha magazeti ya Mwananchi, Mwanaspoti na The Citizen kwa kuanzisha Tuzo ya Mwanasoka Bora.
“Nawapongeza MCL pamoja na gazeti la Mwanaspoti kwamba haliishii kuripoti habari bali hata kusaidia kuinua soka la nchi yetu. Ni kitu kizuri mmekianzisha, naamini kitawapa changamoto mpya vijana wetu na kusaidia kuinua soka letu,” alisema Makamba.

No comments:

Post a Comment