Saturday 16 November 2013

Kocha Zanzibar Heroes aporomosha matusi

KOCHA mkuu wa timu ya taifa ya Zanzibar ‘Zanzibar Heroes’ Salum Bausi anatuhumiwa kumshambulia kwa matusi ya nguoni na kumkashfu mbele ya wachezaji mwandishi wa kituo cha runinga cha Channel Ten, Munir Zakaria, wakati akiwa kazini kwenye uwanja wa Mao Tse Tung kisiwani Zanzibar.
Kwa mujibu wa mashuhuda, mkasa huo ulitokea jana majira ya saa tatu asubuhi, muda mfupi baada ya mwandishi huyo kuingia kwenye uwanja huo akifuatilia mazoezi ya Zanzibar Heroes inayojiandaa na michuano ya Chalenji.
Bausi akiwa tayari amejitayarisha kutaka kumshambulia mwandishi huyo, mwandishi wa ITV, Farouk Karim, aliingilia kati na kumtaka Zakaria kuondoka eneo hilo ili kuepusha shari.
Tanzania Daima ilipomtafuta Zakaria kuhusiana na sakata hilo, alibainisha kuwa Bausi alifanya kitendo hicho kutokana na kumuuliza Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, juu ya uteuzi wa kocha huyo kama ulitokana na ushauri wake wakati wachezaji wakiwa wanampinga.
Zakaria aliongeza kuwa hata hivyo Dk. Shein katika majibu yake, alisema alimshauri Bausi asijiuzulu kutokana na kushindwa kufikia malengo ya kutwaa kombe mwaka jana, na hakutoa maagizo kwa ZFA kuendelea kumchagua kuwa kocha wa timu hiyo.
Juhudi za kumsaka Bausi kuhusiana na tuhuma hizo ziligonga mwamba kutokana na simu yake ya kiganjani kuzimwa

No comments:

Post a Comment