Monday 11 November 2013

Yanga: Tunataka wachezaji hawa watatu


USAJILI wa dirisha dogo utaanza rasmi Ijumaa ijayo. Yanga imedhamiria kuongeza wachezaji watatu kwa nafasi ya straika, kiungo mshambuliaji na beki wa kati.
Hata hivyo Yanga wameweka wazi kwamba timu hiyo itaweka kambi nje ya nchi kujiandaa na mzunguko wa pili na Ligi ya Mabingwa Afrika.
Kambi hiyo, itawekwa katika nchi mojawapo ya Afrika na kama mpango wao utakwenda sawa zaidi watarudi Ulaya kama walivyofanya mwaka jana walipoweka kambi Uturuki.
Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano na Usajili wa Yanga, Abdallah Bin Kleb aliliambia Mwanaspoti kuwa:”Tunataka kujiimarisha kwa kila kitu ili Yanga iwe timu bora si kwa Tanzania tu, bali Afrika kwa ujumla. Kwa hivyo hata wachezaji, watakaoongezwa ni wenye kiwango bora. Tumeshaanza kufanya marekebisho mbalimbali ambayo mwalimu kabla ya kuondoka alituagiza tuyafanyie kazi kwa kuongeza baadhi ya wachezaji.”
“Katika usajili wetu wa dirisha dogo, tutasajili wachezaji watatu na kama wataongezeka, hawatazidi wanne baada ya Kaseja (Juma), tunaowahitaji kwa sasa ni straika, kiungo mshambuliaji na beki wa kati, yeyote atakayekuwa mzuri wa kutufaa tutamsajili.
“Tuna nafasi moja ya mchezaji wa kigeni na huyu ndiye anayeweza kuwa straika au kiungo mshambuliaji na tayari tuna mitego yetu mbalimbali tumeshaiweka kwa ajili ya kukamilisha suala hili,”alisema Bin Kleb na kufafanua sababu ya kumsajili Kaseja kuwa ni uzoefu wake ili awasaidie kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.
Akizungumzia kambi ya timu, Bin Kleb alisema: “Mpango wetu ni kuweka kambi nje ya nchi. Inaweza kuwa nje ya Afrika Mashariki kwa sababu bado tunaendelea na mipango ya kupata mahali pazuri ambapo patakuwa na vifaa na mazingira mazuri.”
“Ndani ya wiki hii, mpango mzima utakamilika kufahamu ni lini na mahali gani tutakwenda, kinachotuchanganya kwa sasa ni haya mashindano ya Chalenji,”alifafanua.
Chalenji inaanza Novemba 27 hadi Desemba 12 nchini Kenya ikihusisha Zanzibar Heroes, Uganda, Burundi, Rwanda na Kilimanjaro Stars ambazo zote zina wachezaji kutoka Yanga.

No comments:

Post a Comment