Saturday 26 October 2013

CCM msipitishe wasio waadilifu- Makamba


Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, ameonya viongozi na watendaji wa CCM nchini kutowapitisha wagombea wasio waadilifu katika chaguzi zijazo kwa sababu itapunguza idadi ya kura huku akiwasisitiza kuliangalia matakwa ya kundi kubwa la wapigakura ambalo ni vijana.
Makamba ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho, aliyasema hayo jana wakati akiwasilisha mada katika mafunzo ya viongozi na watendaji wa CCM nchini (makatibu wa wilaya na mkoa).
Kwa mujibu wa chanzo kutoka ndani ya kikao hicho kilisema “Makamba alisema pamoja na kutekeleza Ilani ya uchaguzi kwa asilimia 100 ama kuwa na ilani nzuri ya uchaguzi bila kuwa na mgombea mwadilifu chama chetu hakitaweza kufanya vizuri katika chaguzi hizo zijazo.”
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Makamba alisemam, wakati wa mkutano mkuu wa chama hicho 2005, Rais Mstaafu Benjamin Mkapa aliwahi kuwaambia wajumbe pamoja na kuangalia ndani ya chama waangalie na nje ya chama wakati wanamchagua mgombea urais.
Imedaiwa kuwa mbunge huyo pia aliwataka viongozi na watendaji wa CCM, kuhakikisha wanasimama upande wa wananchi badala ya watu wachache.
Kuhusiana na makundi ndani ya chama hicho, Makamba alisema makundi hayakuanza wakati wa mfumo wa vyama vingi bali yalikuwapo hata wakati wa chama kimoja.Alisema makundi yaliyopo hivi sasa ni hatari kwa chama kwa sababu ni ya kumbeba mtu na yanaendelea kuwapo hata baada ya uchaguzi.
Chanzo hicho kimesema, Makamba ameshauri kufumuliwa kwa Sekretarieti ya Ajira ya Tamisemi na kuingizwa watendaji wenye machungu na chama. Pia alitaka ajira ndani ya chama hicho zianzie kwa watu wenye elimu ya shahada moja na kuendelea.
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip Mangula, katika mada yake inayohusiana na maadili, aliwaambia viongozi hao kuwa hatakuwa na huruma na watendaji watakaobainika kuwasaidia wagombea wasio waadilifu kupita katika kura za maoni.

No comments:

Post a Comment