Saturday 26 October 2013

Dawa za hospitali zageuzwa dawa za kulevya


Matumizi ya dawa za kulevya nchini yamechukua sura mpya, baada ya kubainika kuwa watumiaji wengi wa dawa hizo aina ya heroin na cocaine sasa wanatumia dawa za hospitali zenye uwezo wa kulevya kuwa mbadala.
Matumizi hayo mabaya yamebainika kutokana na kuwapo ongezeko la matumizi ya dawa za hospitali zilizo na nguvu inayoelezwa kulingana na dawa za kulevya ikiwamo heroin, cocaine na amphetamine.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa ya Uhalifu na Dawa za Kulevya (UNODC) ya mwaka 2013, inathibitisha ongezeko hilo la matumizi ya dawa hizo, ambazo kitaalamu zinaitwa ‘new psychoactive substances (NPS).
“Dawa mbadala za dawa za kulevya zimezua wasiwasi mkubwa siyo kwa sababu ya ongezeko la matumizi yake, bali hata ukosefu wa utafiti wa kisayansi na uelewa wa matumizi yake,” ilisema sehemu ya ripoti ya UNODC.
Katibu Mkuu UNODC, Yury Ferdotov alieleza katika ripoti hiyo ya hali ya dawa za kulevya mwaka 2013 kwamba, changamoto kubwa iliyopo katika kudhibiti dawa hizo duniani ni matumizi ya dawa za hospitali na kemikali zinazotumika kuzitengeneza kutumika kama dawa za kulevya.
Alisema nchi nyingi duniani hazina sheria wala uelewa kuhusu kemikali hizo, jambo linalosababisha wafanyabiashara wakubwa kuendelea kusafirisha kemikali hizo au kutumia teknolojia kulima mimea inayotumika kutengeneza dawa hizo.
UNODC limefafanua kuwa matumizi mabaya ya dawa hutokea wakati dawa za hospitali zinapotumika kwa malengo mengine kinyume na tiba.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa aina tisa ya dawa za hospitali ni miongoni mwa dawa zinzouzwa kwa njia ya panya kama mbadala wa heroin na cocaine.
Dawa hizo ni pamoja na mephedrone, ketamine, benzodiazepine, tramadol na dextromethorphan.
Nyingine ni piperazines, phencyclidines, trypitamines na aminoindance.
Uchunguzi huo umebainisha kwamba unaweza kuzipata dawa hizo kwa wafamasia wasio waaminifu katika hospitali kubwa ambapo huuzwa kwa bei nafuu na wakati mwingine katika maduka ya dawa muhimu.
Mwananchi Jumamosi lilipita katika baadhi ya maduka ya dawa na kufanikiwa kuzinunua dawa hizo zilizothibitishwa kutumika mbadala wa dawa za kulevya bila ya kuwa na cheti cha daktari.

Chanzo Mwananchi

No comments:

Post a Comment