Monday 28 October 2013

Mbuyu Twite ang’ang’ania namba ya Cannavaro


KIRAKA na mchezaji anayetumia nguvu nyingi wa Yanga, Mbuyu Twite ametoa ya moyoni.
Mchezaji huyo raia wa Rwanda ameliambia benchi la ufundi kwamba anacheza vizuri zaidi akisimama katikati na si pembeni anakochezeshwa sasa.
Katika mechi ya Yanga iliyopita dhidi ya Rhino ya Tabora, Twite alisimama kwenye nafasi ya beki wa kati na Kelvin Yondani baada ya Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kutokuwepo na sasa amesisitiza kuwa anajisikia raha zaidi akiendelea kusimama hapo.
Twite amekuwa akichezeshwa nafasi ya beki wa kulia wa Yanga ingawa ana uwezo wa kucheza pia kushoto na kwenye kiungo akiwa na maana kwamba anataka kucheza katikati ama kwenye nafasi ya Yondani au ya Cannavaro.
“Katika namba zote, nafurahia zaidi ninapocheza beki wa kati namba nne na tano, ni nafasi ninayoipenda kuliko nyingine zote na kiukweli ninapopangwa hapo huwa naifurahia kucheza.”
“Lakini pamoja mapenzi yangu, huwa sichagui nafasi ya kucheza, mahali popote ambako kocha atanipanga niko tayari iwe kulia, kushoto, kiungo kokote sawa, anayejua anajua tu, lakini ningefanya kazi vizuri zaidi pale katikati,”alisema Twite na kuongeza kwamba yeyote atakayepangwa naye kwenye ulinzi atapiga naye kazi wala habagui kwavile amefanya nao mazoezi na anawajua.
Tangu ametua Yanga msimu uliopita, amekuwa beki wa kulia wa kudumu ingawa mara nyingine kunapotokea mapungufu kwenye nafasi ya beki wa kati inayochezwa na Cannavaro na Kelvin Yondani au kiungo mkabaji.
Twite ndiye aliyeanza kumuweka benchi nahodha wa Yanga aliyetemwa, Shadrack Nsajigwa. Benchi la ufundi lilimpa kipaumbele Twite kwavile ana uwezo wa kucheza namba zaidi ya moja na kusaidia timu kwa lolote linaloweza kutokea ndani ya dakika 90.

No comments:

Post a Comment