Friday 25 October 2013

Rais wa Uswisi aifunda Tanzania jinsi ya kupata fedha za kifisadi


Katika mahojiano maalumu na timu ya waandishi wa Mwananchi na The Citizen jana, Graf alisema kuwa Serikali ya Tanzania inapaswa kusaini mkataba wa kimataifa wa kubadilishana taarifa za masuala ya usimamizi wa fedha na kodi ili kuweza kujua ni kina nani wameweka fedha nchini kwake na kunufaika na kodi.
Graf, ambaye alikuwa katika ziara ya kikazi nchini, alisema kuwa hivi karibuni Serikali ya Uswisi ilisaini mkataba wa kimataifa wa kubadilishana taarifa kuhusu masuala ya fedha, ambao unajulikana kwa lugha ya Kiingereza kama `Convention on Mutual Administrative Assistance in Tax Matters’.
Alisema ikisaini mkataba huo ina maana itasaidiwa na Serikali ya Uswisi kupata fedha zilizofichwa na Watanzania.
“Serikali ya Tanzania inatakiwa kuweka mkakati wa kisheria utakaotengeneza mazingira ya kubadilishana taarifa za fedha na mataifa mengine. Kwa jambo hilo hata Serikali ya Uswisi inaweza kusaidia katika kupatikana kwa fedha zilizofichwa,” alisema Graf, ambaye anaongoza Serikali ya Uswisi kwani kwa kawaida Rais wa Bunge ndiye pia kiongozi wa taifa hilo.
Graf alisema kwa sasa itakuwa ngumu kwa Tanzania kupata fedha hizo kwani haijasaini mkataba wa kimataifa wa kubadilishana taarifa za fedha na mataifa mengine.
Alieleza pia katika miaka ya karibuni Serikali ya Uswisi imeandaa muswada wa sheria wa kubana fedha zilizopatikana kwa njia za kifisadi na kufichwa katika benki za Uswisi. Graf alisema sheria hiyo ikipita itaruhusu Serikali ya nchi hiyo kutaifisha fedha ambazo zimepatikana kwa njia haramu na kufichwa katika benki za huko.
Muswada huo unaoitwa kwa lugha ya Kiingereza `Freezing and Restitution of Assets of Politically Exposed Persons obtained by Unlawful Means Bill’ ulisomwa kwa mara ya kwanza kwenye Bunge la nchi hiyo mwezi Mei, mwaka huu.
Graf alisema faida nyingine ya Tanzania kusaini mkataba huo ni kuwa, itaweza kuwatoza kodi Watanzania hao walioweka fedha huko.
Alifafanua kuwa siyo fedha zote zinazowekwa kwenye benki za Uswisi kuwa ni haramu kwani kuna nyingine zimepatikana kihalali, lakini zinaweza kutozwa kodi.
“Tanzania inakosa kodi kutokana na fedha zilizohifadhiwa na Watanzania wenye akaunti kwenye benki za Uswisi,” aliongeza Graf, ambaye alichaguliwa kuwa Rais wa nchi hiyo Novemba 26, 2012 na kutakiwa kukaa madarakani kwa mwaka mmoja.
Graf alisema pia fedha za kodi zingeisaidia Tanzania kugharimia sekta mbalimbali za maendeleo.

Chanzo Mwananchi

No comments:

Post a Comment