Friday 25 October 2013

Rage akataa kugombea Simba












MWENYEKITI wa Simba, Ismail Aden Rage, amesema hatogombea tena uongozi katika klabu hiyo kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Akizungumza na Mwanaspoti juzi Jumanne, Rage, alisema kwamba ameshangazwa na hatua ya baadhi ya watu wanaotaka uongozi kuanza harakati hizo kwa kuihujumu timu.
Alisema anajua watu hao wanamhofia yeye na ndio maana wameamua kuanza mapema mikakati yao ya kuwania uongozi kwa kuihujumu klabu wakiamini ndio njia ya kummaliza, lakini amewatoa hofu kwa kusema yeye hatogombea.
“Ninapenda niwaambie wanaonihofia kuwa, sitagombea tena. Lakini napenda pia kusema kuwa wanaotaka uongozi wajue kwamba zama za uongozi wa dezo zimekwisha,’’ alisema Rage.
Alisema kwamba anachokifanya kwa wakati huu ni kuweka mazingira mazuri katika klabu hiyo na wiki ijayo ataitisha mkutano wa katiba.
Rage aliingia madarakani Mei, 2010 kwa kura 785 akimbwaga, Hassan Hassanol aliyepata kura 435. Kwa mujibu wa Katiba ya Simba, uchaguzi mkuu ujao unatakiwa ufanyike Mei, 2014.

No comments:

Post a Comment