Sunday 18 August 2013

‘CCM imevunja Muungano’

Kutoka mkoani Kagera, mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, amesema kuwa CCM tayari imeuvunja Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kutokana na muundo wa Katiba mbili za Muungano na ile ya Zanzibar.
Akiwahutubia wanachi waliohudhuria mikutano ya mabaraza ya wazi ya CHADEMA ya kujadili rasimu ya Katiba mpya
mjini Bukoba, Lissu alisema kuwa Katiba hizo mbili zinaonyesha mkanganyiko wa wazi unaovunja Muungano.
Alisema kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano inatamka wazi katika ibara yake ya kwanza kwamba Tanzania ni nchi moja ya Jamhuri ya Muungano, wakati ile ya Zanzibar nayo inatamka kuwa Zanzibar ni nchi, hivyo kuzifanya ziwe nchi mbili zenye madaraka kamili.
“Tanzania si nchi moja kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar, kwa sababu Muungano ulioasisiwa na Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Aman Karume, tayari umekufa na CCM ndiyo imeuua,” alisema.
Lissu alifafanua kuwa Zanzibar tayari ina alama zake ikiwemo wimbo wa taifa, rais wake ambaye ni mkuu wa vikosi vya idara maalumu, mahakama yake na bendera yake.
“Kuna haja sasa kufufuka Tanganyika kama Tume ya Jaji Warioba ilivyopendekeza kuwa na serikali tatu. Leo Jamhuri ya Watu wa Zanzibar imefufuliwa, kwa maana hiyo hakuna budi pia kufufuliwa kwa Jamhuri ya Tanganyika kutoka katika ‘wafu’,” alisema.


Chanzo Mwananchi

No comments:

Post a Comment