Sunday 18 August 2013

HAAA! MASKINI KASEJA






Mkongo’ wa Kaseja anusurika

Mwakilishi wa Timu ya Soka ya FC Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Ismael Balanga Bandua, amenusurika kufungwa jela kwa kuishi nchini bila kibali, baada ya kutiwa hatiani na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa makosa hayo.
Bandua ambaye alifika nchini hivi karibuni kwa lengo la kukamilisha taratibu za timu hiyo kumsajili kipa wa zamani wa Simba, Timu ya Taifa (Taifa Stars), Juma Kaseja alipatikana na hatia hiyo jana baada ya kukiri kutenda makosa hayo.
Baada ya kusomewa mashtaka, Mkongo huyo alikiri kutenda makosa hayo, lakini akajitetea kuwa alikuwa hajui sheria za Tanzania.
Kutokana na kukiri kwake makosa hayo, Hakimu Mkazi Hellen Riwa alimhukumu kifungo cha miezi mitatu jela, ama kulipa faini ya Sh50,000.
Alinusurika kutupwa jela, baada ya kufanikiwa kulipa faini hiyo ya Sh50,000 iliyochangwa na watu wanaosadikiwa kuwa ni ndugu zake walioko hapa nchini kihalali.
Alipandishwa kizimbani mahakamani hapo jana na kusomewa mashtaka ya kuishi nchini bila kibali kinyume cha kifungu cha 31(1)(i) na (2) cha Sheria ya Uhamiaji, Sura 54, kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Katika kesi hiyo, Wakili wa Uhamiaji, Patrick Ngayomela, pia alidai kuwa Mkongo huyo anakabiliwa na shtaka la kuwapotosha maofisa Uhamiaji.
Chanzo Mwananchi

No comments:

Post a Comment